Δευτέρα 12 Οκτωβρίου 2015

Kuongezeka mgogoro wa usalama wa chakula barani Afrika


"...Licha ya kuwa nchi nyingi za bara la Afrika zina utajiri mkubwa wa maliasili kama vile almasi na dhahabu lakini ni asilimia 29 tu ya watu wa bara hilo ndio wanaonufaika na umeme na asilimia 65 kunufaika na mahitaji ya msingi maishani kama vile maji ya kunywa..."

Iran Swahili Radio

Kuongezeka mgogoro wa usalama wa chakula barani AfrikaUhaba wa vyanzo vya chakula na ukame unaoshuhudiwa katika nchi nyingi za bara la Afrika ni mambo ambayo yamezipelekea nchi hizo kukabiliwa na mgogoro wa kutokuwepo usalama wa chakula kwa kadiri kwamba, mashirika mengi ya kimataifa yanayoshughulikia misaada ya kibinadamu ukiwemo Mpango wa Chakula Duniani WFP, yameonya juu ya uwezekano wa kutokea janga la uhaba wa chakula na baa la njaa katika nchi hizo. Katika ripoti yake ya hivi karibuni kabisa, WFP imeonya kuwa watu milioni 27 wa nchi za kusini mwa bara la Afrika hawana usalama wa chakula. Mpango huo wa chakula unasema katika kipindi cha mwaka wa 2015-2016 asilimia 16 ya watu wa Zimbabwe au kwa ibara nyingine watu milioni moja na nusu wa nchi hiyo wanakabiliwa na tatizo la uhaba wa chakula na baa la njaa. Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa na Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika SADC, mazao ya mahindi nchini Zimbabwe mwaka huu yamepungua kwa tani laki 7.42 yakilinganishwa na ya mwaka uliopita. Mpango wa WFP na Shirika la Kuhudumia Watoto la Umoja wa Mataifa UNICEF yametabiri kuwa kufikia mwishoni mwa mwaka huu, raia wapatao milioni nne na nusu wa Ethiopia watahitaji misaada ya chakula, na kwamba nchi hiyo inahitaji msaada zaidi wa dola milioni 230 ili kukabiliana na hali hiyo.
Wataalamu wanasema kutokea kwa ukame wa msimu katika baadhi ya maeneo ya bara la Afrika kumepunguza sana mazao ya kilimo yakiwemo mahindi katika maeneo hayo. Vilevile wanasema kupungua kwa malisho ya mifugo kumesababisha upungufu wa bidhaa zinazotokana na wanyama hao ikiwemo nyama na hivyo kuzidisha bei ya bidhaa hizo sokoni. Vilevile kuzuka magonjwa ya kuambukiza na mapigano ya ndani katika baadhi ya nchi za Kiafrika kumepelekea wafugaji na wakulima wengi kuyakimbia mashamba yao na kutafuta usalama kwingineko.
Wajuzi wa mambo wanasema licha ya kuwa baadhi ya nchi za Kiafrika kwa miaka mingi zimekuwa na mipango ya kutumia teknolojia ya kisasa kwa shabaha ya kuimarisha mazao yao ya kilimo lakini mipango hiyo haijatekelezwa kutokana na ughali wa mitambo na mashine za kuifanikisha na pia hatua ya nchi tajiri za Magharibi ya kutotoa msaada wowote katika uwanja huo.
Mbali na Zimbabwe na Ethiopia, Zambia, Botswana na Malawi ni nchi nyingine za kusini mwa Afrika ambazo zinakabiliwa na tatizo la upungufu mkubwa wa chakula. Mbali na nchi hizo migogoro ya kisiasa na mapigano yanayoendelea huko Sudan Kusini, Somalia na nchi nyingine nyingi za Kiafrika si tu kuwa ni mambo yanayohatarisha pakubwa usalama wa chakula barani Afrika bali pia yanavuruga shughuli za masharika ya kimataifa ya misaada za kuwafikia wahanga wa migogoro hiyo. Uhaba wa umeme na maji na vilevile uchumi dhaifu ni mambo mengine yanayosemekana kuchangia upungufu wa mazao katika sekta tofauti ikiwemo ya kilimo barani Afrika. Licha ya kuwa nchi nyingi za bara la Afrika zina utajiri mkubwa wa maliasili kama vile almasi na dhahabu lakini ni asilimia 29 tu ya watu wa bara hilo ndio wanaonufaika na umeme na asilimia 65 kunufaika na mahitaji ya msingi maishani kama vile maji ya kunywa.
Wataalamu wanasema kuwa katika miongo michache inayokuja, dunia kwa kuongezeka idadi ya watu itakabiliwa na changamoto kubwa za maji na chakula. Hii ni katika hali ambayo bara la Afrika lina asilimia 60 ya ardhi za kilimo zisizotumika, ambapo kutumiwa vyema kwa ardhi hizo kunaweza kuwa na mchango mkubwa na muhimu si tu katika kudhamini usalama wa chakula wa bara hilo tu bali wa ulimwengu mzima kwa ujumla.
Kwa msingi huo ni wazi kuwa kumalizwa mivutano na mapigano pamoja na kuboreshwa kwa miundombinu ya bara la Afrika si tu ni jambo la dharura katika jitihada za kulikomboa bara hilo kutokana na umasikini wa chakula bali pia katika kupunguzwa umasikini katika upeo wa kimataifa.

Δεν υπάρχουν σχόλια:

Δημοσίευση σχολίου