Τρίτη 6 Οκτωβρίου 2015

Maaskofu Orthodox watakatifu watatu: Basili Mkuu, Yohane Krisostomo na Gregori wa Nazianzo


Basili wa Kaisarea
 
Sw.wikipedia
 
Basili wa Kaisarea (Kaisarea wa Kapadokia, leo Kayseri, nchini Uturuki, takriban 329 – Kaisarea wa Kapadokia, 1 Januari, 379) alikuwa mmonaki, halafu askofu wa mji huo (mkoa wa Kapadokia, leo nchini Uturuki).
Ni mmojawapo kati ya Mababu wa Kanisa muhimu zaidi. Ndiyo sababu anaitwa Basili Mkuu (kwa Kigiriki Βασίλειος ο Μέγας).
Kwa jinsi alivyomkazia macho Kristo na kupenda watu, alianza kuheshimiwa kama mtakatifu punde baada ya kifo chake.
Sikukuu yake inaadhimishwa kila mwaka tarehe 1 Januari.


Picha takatifu ya Kirusi ya Mt. Basili.

Maisha
 

Asili na ujana

 

Basili alizaliwa mwaka 329 hivi katika familia tajiri ya mhubiri maarufu Basili Mzee na ya Emelia wa Kaisarea huko Caesarea Mazaca. Wote wawili walijulikana kwa imani yao (Oratio 43.4, PG 36. 500B).
Familia yao ilikuwa na watoto 10, waliosaidiwa malezi na bibi wa Basili, Makrina Mzee. Babu yake alikuwa mfiadini. Wote wawili wanaheshimiwa kama watakatifu, kama vile Basili na watoto wengine 4: dada yake Makrina Kijana aliyekuwa mmonaki, na ndugu zake Petro wa Sebaste aliyekuwa askofu na mwanateolojia huko Armenia, Naukratio aliyekuwa mkaapweke, na hasa Gregori wa Nisa ambaye alifanywa na Basili kuwa askofu wa mji huo akaandika vitabu bora kuhusu teolojia na maisha ya Kiroho.
Basili alikuwa na vipawa vya pekee: akili kali, wema mkubwa, uwezo wa kupanga na kufanikisha mambo, nguvu katika utendaji, busara na kiasi katika yote. Ni kati ya wanakanisa kamili zaidi wa nyakati zote.
Bado mtoto alihamia mkoa wa Ponto hadi alipofiwa baba yake ambapo akarudi Kaisarea ili kupata wlimu. Huko alikutana na Gregori wa Nazianzo, akawa rafiki yake maisha yake yote.
Wote wawili walikwenda kusoma Konstantinopoli, halafu kwa miaka sita Athens, walipokutana na atakayekuwa kaisari Juliano Mwasi. Ndiko alikoanza kufikiria maisha ya Kikristo hasa. Hata hivyo hakuacha kutia maanani elimudunia, aliyokuwa nayo kwa wingi, hasa kwa ajili ya malezi ya vijana, ambao daima aliwashughulikia sana.
Kutokana na mang’amuzi yake kuhusu vitabu vya Wapagani wa zamani, alihimiza upambanuzi: “Tukiwa na hekima, tutachota katika maandishi hayo vile ambavyo vinatufaa na vinalingana na ukweli, na tutapuuzia vile vingine.”
Alipohama Athens mwaka 355 hivi, Basili alifanya kwa muda mfupi kazi ya wakili na mwalimu wa kuhubiri huko Kaisarea, lakini mwaka uliofuata alibadili maisha kisha kukutana na askofu Eustathius wa Sebaste.
Aliandika, “Siku moja, kama mtu aliyezinduka kutoka usingizi mzito, niligeuza macho yangu kwenye mwanga wa ajabu wa ukweli wa Injili… nikalia machozi mengi juu ya maisha yangu duni”. Hapo, kwa kuvutiwa na Yesu, alianza kumtazama na kumsikiliza yeye tu, akijitosa katika sala, tafakuri juu ya Biblia na maandishi ya mababu wa Kanisa, pamoja na kutekeleza upendo, kwa kufuata pia mfano wa dada yake, Makrina, aliyekwishashika maisha ya kimonaki.

Umonaki

 

Baada ya kupata ubatizo, Basili alisafiri tena (357) kwenda Misri, Palestina, Syria na Mesopotamia ili kufahamu zaidi maisha ya kiroho na umonaki.
Ingawa aliguswa na utakatifu wa wamonaki aliokutana nao huko, kipeo cha ukaapweke hakikumvutia zaidi. Badala yake alielekea maisha ya kijumuia. Hivyo baadaye alirekebisha umonaki usiwe mbali mno na watu wa kawaida, bali uathiri maisha yao kwa roho ya Kikristo.
Kiongozi halisi katika njia ya Mungu, hakuruhusu malipizi ya ajabuajabu, bali alidai utekelezaji wa matendo ya upendo.
Kisha kugawa mali zake kwa mafukara alikwenda kwa muda mfupi kuishi upwekeni karibu Neokaisaria mtoni Iris, lakini mwaka 358 alianza kupokea wafuasi, mmojawao ndugu yake Petro. Pamoja naye alianzisha monasteri huko Arnesi kwenye mkoa wa Ponto.
Huko walijiunga hata mama yake, dada yake Makrina na wanawake wengine, wakijitoa kusali na kutekeleza matendo ya huruma.
Ni huko kwamba Basili aliandika vitabu vyake kuhusu umonaki (Kanuni mbili) vilivyoathiri Kanisa lote hadi leo, hata akaitwa "baba wa umonaki wa mashariki". Benedikto wa Nursia mwenyewe, “baba wa umonaki wa magharibi”, alimhesabu kama mwalimu wake. Kwa jumla mfumo wa umonaki haueleweki bila kumsikiliza Basili.
Mwaka 358 alimualika Gregori wa Nazianzo ajiunge naye, halafu kwa pamoja walitunga Filocalia, mkusanyo wa maandishi bora ya Origen. Baadaye Gregori akarudi kwao.
Basili alishiriki Mtaguso wa Konstantinopoli wa mwaka 360 alipokubali neno "homoiousios" kama sahihi kuelezea Yesu ni "kama" Mungu Baba, si "sawa" wala si "tofauti" naye. Baada ya kulaumiwa na askofu wake, Dianius wa Kaisarea, aliacha mtazamo huo akashika moja kwa moja Kanuni ya imani ya Nisea.

Daraja takatifu

 

Picha takatifu ya Maaskofu watakatifu watatu: Basili Mkuu (kushoto), Yohane Krisostomo (katikati) na Gregori wa Nazianzo (kulia) kutoka Lipie, Historic Museum huko Sanok, Poland.
 
Mwaka 362 Basili alipewa daraja takatifu ya ushemasi kwa kuwekewa mikono na askofu Meletius wa Antiokia.
Aliitwa na Eusebius arudi kwao, akapewa upadirisho mwaka 365.
Miaka iliyofuata Basili na Gregori walishindana na uzushi wa Ario ulioenea Kapadokia. Katika midahalo wakawa washindi.
Hivyo Basili alikabidhiwa usimamizi wa mali ya dayosisi ya Kaisarea. Eusebius akamuonea kijicho akamruhusu arudi upwekeni. Lakini Gregori alimshauri arejee tena na kushika nafasi yake kama kiongozi halisi wa jimbo hilo.
Mwaka 370 Eusebius alifariki, na Basili alichaguliwa mwandamizi wake akapewa uaskofu tarehe 14 Juni 370. Kama askofu wa Kaisarea akawa pia askofu mkuu mwenye majimbo 5 chini yake.
Hapo alikataa katakata mashinikizo ya Kaisari aliyetaka aunge mkono uzushi wa Ario, kinyume chake alijitahidi kurudisha umoja ndani ya Kanisa na kutetea haki ya kushika imani ya kweli kuhusu umungu wa Yesu.
Alitetea pia umungu wa Roho Mtakatifu ambaye aliandika kitabu kizima juu yake: “lazima alinganishwe na kutukuzwa pamoja na Baba na Mwana”. Hivyo Basili ni kati ya mababu walioweka wazi fundisho la Utatu Mtakatifu: Mungu pekee, kwa kuwa ni upendo, ni nafsi tatu zinazounda umoja wa Kimungu, imara kuliko umoja wowote.
Pamoja na kuchunga kiroho waamini wa jimbo lake kubwa, na kujitahidi kuleta watu wote kwa Kristo, alizingatia mahitaji ya kimwili ya kila mmoja, akajitosa kwa ajili ya maskini, wezi na makahaba, akihimiza watawala kuinua hali ya wananchi hasa wakati wa maafa, na akilaumu hadharani walioshindwa kutoa hukumu kwa haki.
Alianzisha mtaa wenye majengo kwa ajili ya mafukara, wageni na wagonjwa, uliokuja kuitwa Basiliade. Ulikuwa na hospitali, shule na viwanda.
Hata katika makanisa mengine yaliyokuwa chini yake alianzisha makimbilio kwa shida yoyote ile.
Kama askofu, alianzisha maisha ya pamoja katika “jamaa” kwa lengo la kushika kikamilifu udugu wa Kiinjili kama katika Kanisa la mwanzoni.
Tofauti na monasteri za Pakomi, zilizofikia kuwa na watawa elfu, jamaa hiyo haikuwa na idadi kubwa wala ngome; tena haikuwa jangwani, bali karibu na mji wa Kaisarea wa Kapadokia.
Akiwa askofu huko alitembelea mara nyingi jamaa hizo akisisitiza, pamoja na maendeleo ya kiroho, uhusiano na Kanisa lao: alitaka watawa wa kiume na wa kike wawe chachu inayofanya Wakristo wenzao wote wafuate utakatifu wa wito wao. Tena aliwakabidhi shughuli mbalimbali kama vile kuhubiri na hasa kuhudumia wenye shida.
Mtindo huo ulisisitiza ushirikiano kati ya ndugu kuliko uongozi wa abati na miundo mikubwa.
Tofauti na unyofu wa wamonaki wa jangwani, alitia maanani masomo ya kidini, na hasa maandishi ya Origene.
Mpaka leo kanuni zake zinaongoza karibu monasteri zote za mashariki, na kwa njia hiyo makanisa ya Kiorthodoksi kwa kuwa kwao maaskofu kwanza ni wamonaki, nao wanaelekeza Wakristo wote kufuata mifano yao.
Mhubiri mwenye nguvu, alishambulia uroho wa matajiri na ulegevu wa Wakristo wasiotimiza wajibu wao.
Pamoja na kuwajibika mfululizo kutekeleza matendo ya huruma, alirekebisha pia liturujia ya Ekaristi na kustawisha matumizi ya Zaburi kati ya waamini, kiasi kwamba walizisali hata usiku; na kuhimiza waamini wapokee kila siku Ekaristi, chakula wanachohitaji ili kupata nguvu mpya ya kuishi kikamilifu kadiri ya neema ya ubatizo. Alisema ni furaha kubwa kuweza kushiriki Ekaristi iliyowekwa “ili kudumisha bila kikomo kumbukumbu ya Yule aliyekufa na kufufuka kwa ajili yetu”.
Alipanga maisha ya Kanisa bila kukubali serikali iyaingilie.
Alipodaiwa na mjumbe wa Kaisari Valens alegeze msimamo wake dhidi ya Ario, Basili alimjibu, "Labda wewe hujawahi kuhusiana na askofu yeyote." Baada ya jibu hilo kwa Kaisari alikwenda kushiriki misa yake akampe eneo kwa ajili ya Basiliade. Tukio hilo lilisaidia kuonyesha mipaka kati ya mamlaka ya serikali na ile ya Kanisa.
Basili aliwasiliana pia na [orthodox] Papa Damaso I ili Kanisa la Roma litumie mamlaka yake kulaani uzushi wa Ario,mashariki kama magharibi.
Lakini hakuishi kirefu kutosha aone ushindi wa imani sahihi aliyotetea. Juhudi zake kubwa za kutimiza vizuri wajibu wake kama askofu zilimmaliza tarehe 1 Januari 379, akiwa na umri wa miaka 49 tu.
Katika Kanisa alitekeleza kiaminifu mpango alioufanya mapema, wa kuwa “mtume na mtumishi wa Kristo, msimamizi wa mafumbo ya Mungu, mtangazaji wa Ufalme, kielelezo na kipimo cha uadilifu, jicho la Mwili wa Kanisa, mchungaji wa kundi la Kristo, mwalimu, baba na tabibu mpendevu, mfanyakazi pamoja na Mungu, mkulima wa Mungu, mjenzi wa hekalu la Mungu”.

Mafundisho yake

Mwanga wa fumbo la Mungu unarudishwa na binadamu aliye sura yake; ni hasa kwa kumtazama Kristo kwamba tunaweza kutambua hadhi yetu. “Zingatia ukuu wako, ukikumbuka ulivyogharimiwa: tazama bei ya ukombozi wako na kuelewa hadhi yako!”
Kwa namna ya pekee Wakristo wakijilinganisha na Injili, wanapaswa kuwatambua watu wote kama ndugu, tena kujiona wasimamizi wa mali waliyojaliwa ili wawajibike kila mmoja kwa ajili ya wenzake, “wakitekeleza maagizo ya Mungu mfadhili”. “Macho ya mafukara wote yanaelekea mikono yetu kama vile ya kwetu yanavyoelekea ile ya Mungu tukiwa na shida”.
Kuhusu hilo alitumia kishujaa maneno makali katika hotuba zake, kwa sababu anayetamani kumpenda jirani kama anavyojipenda, kadiri ya amri ya Mungu “hatakiwi kuwa na mali yoyote kuliko jirani yake”. Hasa wakati wa maafa alihimiza waamini wasiwe “wakatili kuliko hayawani… kwa kujipatia vile ambavyo wote wanamiliki kwa pamoja au kwa kuteka vitu vilivyo mali ya wote”.

Maandishi yake

  • On the Holy Spirit
  • Refutation of the Apology of the Impious Eunomius
  • Refutation (vitabu 3 vya kwanza tu)
  • Hexaëmeron
  • Ufafanuzi wa Zaburi
  • Moralia
  • Asketika
  • Barua 300

Tafsiri ya Kiswahili

  • MT. BASILI WA KAISARIA, Kanuni za kimaadili – tafsiri ya Familia za Maamkio – Mapanda - ed. Ndanda Mission Press – Ndanda 2005 – ISBN 9976-63-674-X
Vyanzo
Kwa Kiswahili
Kwa lugha ntyingine
Viungo vya nje
 Basil the Great article from Orthodox Wikipedia has a slightly longer article on St. Basil

Gregori wa Nazianzo

Sw.wikipedia
 
Gregori wa Nazianzo (Arianzo, leo Güzelyurt nchini Uturuki, 329 - Arianzo, 25 Januari 390) alikuwa askofu, mwanateolojia na mwanashairi maarufu kutoka katikati ya nchi ambayo leo inaitwa Uturuki.
 

Maisha

Mchoro wa Andrei Rublev, Gregory the Theologian (1408), kwenye kanisa kuu la Bikira Maria Kulala, huko Vladimir (Urusi).

 

Asili na utoto

 

Alizaliwa mwaka 329 huko Arianzo, kijiji karibu na Nazianzo, mkoani Kapadokia, katika familia ya kisharifu ya watakatifu. Baba yake aliitwa Gregori mzee na mama yake Nonna.
Baba, aliyekuwa Myahudi, aliongokea Ukristo kwa msaada wa mke wake na hatimaye akawa askofu wa Nazianzo.
Gregori, aliyezaliwa miaka 4 baada ya Mtaguso wa kwanza wa Nisea (325) uliolaani uzushi wa Ario, aliathiriwa na mapambano hayo ya kiimani maisha yake yote.
Mwenye akili kali na ubunifu mkubwa, alielekea sana upweke na maisha ya sala, lakini wema na ari yake, pamoja na ufasaha wa ajabu wa mahubiri yake vilimrudisha kati ya watu. Ila alipokabiliana na upinzani mkali, moyo wake mpole na mwepesi kuguswa ulimfanya akimbilie tena upwekeni.
Kuhusu mwelekeo huo aliandika: “Sioni kitu kikuu kuliko hiki: kunyamazisha hisi zangu, kuinuka juu ya mwili wa ulimwengu, kujifungia ndani mwangu, kutoshughulikia tena mambo ya kibinadamu isipokuwa ya lazima kabisa; kuongea na nafsi yangu na Mungu, kuendesha maisha yanayopita vitu vinavyoonekana, kubeba rohoni taswira za Kimungu, safi daima, zisizochanganyikana na maumbo ya kidunia au madanganyifu, kuwa kweli kioo kamili cha Mungu na cha mambo yake, tena kuwa hivyo zaidi na zaidi, kwa kuchota mwanga kutoka mwanga… kufurahia kwa tumaini la sasa mema yajayo na kuongea na malaika, kuwa nimeacha tayari dunia ingawa naishi bado juu yake, nikiinuliwa na roho”.

 

Ujana

 

Alisoma kwanza huko Kaisarea wa Kapadokia, alipofunga urafiki wa kudumu na Basili Mkuu, halafu katika vyuo bora vya wakati ule: Kaisarea ya Palestina, Aleksandria ya Misri, Konstantinopoli na hatimaye (350 - 357) huko Athens, Ugiriki.
Aliporudi kwao tu, ndipo alipobatizwa, ingawa mama yake alikuwa amemtoa kwa Mungu siku ileile ya kuzaliwa.

 

Mtawa na padri

 

Baada ya kujiunga na Basili (358) kwenye monasteri ya Annisoi, katika mkoa wa Ponto, na kumsaidia kutunga Filokalia, alirudi nyumbani alipotarajia kuishi upwekeni zaidi. Kumbe mwaka 361 baba yake aliamua kumpa upadrisho. Kwanza alikimbia, lakini baadaye alikubali kufuata maongozi ya Mungu yaliyozidi kumpeleka asikotaka mwenyewe, na akishinda silika yake ya aibu alitumia vipawa vyake kama mwandishi na mhubiri mahiri kwa ajili ya Kanisa.
Alisema, “Kama mtumishi wa Neno, nawajibika katika huduma ya Neno; nisikubali kamwe kuzembea katika jema hilo. Nathamini wito huo na kushukuru kwa ajili yake; unanipa furaha kuliko mambo mengine yote pamoja”..

 
Yohane Krisostomo na Gregori wa Nazianzo
katika picha ya Kirusi ya karne XVIII.

 

Askofu

 

Mwaka 372 Basili, akiwa askofu mkuu wa Kaisarea wa Kapadokia, alimteua kuwa askofu wa Sasima. Kutokana na upinzani wa Kaisari, Gregori hakuweza kwenda kamwe, akatawa huko Seleukia, lakini alipofiwa baba yake alirudi Nazianzo, aongoze Kanisa la huko.
Mwaka 379 aliitwa aongoze Wakristo wachache wa Konstantinopoli walioshika Kanuni ya imani ya Nisea. Majengo yote yalikuwa yanamilikiwa na Waario walioungwa mkono na serikali. Lakini Theodosius I alipotawazwa kama Kaisari mwaka 380 aliyatoa kwa hao Waorthodoksi.
Jijini huko dhidi ya upinzani uliomzunguka, alitetea na kufafanua imani katika Utatu Mtakatifu kwa hotuba tano zilizomstahilia jina la "Mwanateolojia". Mwenyewe alieleza kuwa "teolojia" si "teknolojia", yaani haitegemei hoja za binadamu, bali inatokana na maisha ya sala na utakatifu.
Udhati wa mafundisho pamoja na uzuri wa namna yalivyotolewa zinafanya hotuba hizo zituvutie hata leo.
Theodosius I alimtawaza Patriarki wa Konstantinopoli na kuhakikisha kwamba atambuliwe hivyo na Mtaguso wa kwanza wa Konstantinopoli mnamo Mei 381.
Majadiliano katika huo mtaguso mkuu yalikuwa makali hata dhidi yake, kwa sababu alitetea kwa nguvu umungu wa Yesu Kristo na wa Roho Mtakatifu, kwa hiyo pia dogma ya Utatu mtakatifu.
Alionja kwa mara nyingine alichokuwa amekilaumu kama mpenzi wa amani: “Tumemgawa Kristo, sisi tuliowapenda hivi Mungu na Kristo! Tumeambiana uongo kwa sababu ya Ukweli, tumefuga hisia za chuki kwa sababu ya Upendo, tumetengana kati yetu”.
Hatimaye, akikiri hawezi kusuluhisha, aliacha mtaguso aliokuwa anauendesha akaaga waamini katika kanisa kuu lililokuwa limejaa kabisa.

 

Miaka ya mwisho

 

Mwishoni mwa mwaka 382 akawa askofu wa Nazianzo lakini, baada ya mwaka mmoja, alirudi upwekeni Arianzo, alipofariki tarehe 25 Januari mwaka 389 au 390.
Ni katika miaka hiyo ya mwisho, aliyoitumia katika masomo na maisha ya kiroho, kwamba aliandika sehemu kubwa ya mashairi yake, na hasa maisha yake mwenyewe, akipitia safari yake ya kiutu na ya Kikristo kama mtu wa Mungu aliyeonja mateso mengi katika ulimwengu uliojaa mabishano.
Mafundisho yake kuhusu Kristo, yanayotetea pia usahihi wa jina “Mama wa Mungu” kwa Bikira Maria, yalikuja kupitishwa na Mtaguso wa Efeso (431) na Mtaguso wa Kalsedonia (451).
Kama mwanashairi na mwanafasihi alitoa maandishi bora kuhusu imani. Zimetufikia hotuba 45, mbali ya tenzi (karibu beti 18,000!) na barua nyingi sana.

Mafundisho yake

Gregori alihimiza kwanza sala, akisema, “Ni lazima tumkumbuke Mungu mara nyingi kuliko tunavyopumua”, kwa kuwa sala ni mkutano wa kiu ya Mungu na kiu yetu: yeye ana kiu ya kutuona tuna kiu naye. Katika sala tunapaswa kuelekeza mioyo yetu kwake, kujiaminisha kwake kama sadaka ya kutakaswa na kugeuzwa. Katika sala tunaona vyote katika mwanga wa Kristo, tunaacha vinyago tunavyojifunika vianguke na tunazama katika ukweli na katika kumsikiliza Mungu, tukichochea moto wa upendo.
Pia alisisitiza ukamilifu wa utu wa Yesu, ukiwa pamoja na roho ya kibinadamu, kama sharti la wokovu wetu: “Kisichowahi kutwaliwa hakijaponywa”. Kama yeye “asingekuwa na akili inayoweza kufikiri, angekuwaje mtu?” Kumbe, kwa kujifanya kweli mtu, ametuwezesha kuwa kama yeye: “Tujitahidi kuwa kama Kristo, kwa sababu Kristo naye amekuwa kama sisi: kugeuka miungu kwa njia yake, kwa sababu mwenyewe amekuwa mtu kwa njia yetu. Alijitwalia yaliyo duni zaidi ili atuzawadie yaliyo bora”.
Bikira Maria, aliyempa Kristo umbile la mtu, ni kweli Mama wa Mungu; na kwa ajili ya kazi hiyo muhimu sana “alitakaswa kabla ya wakati". Yeye ni kielelezo na msaidizi wa kumkimbilia katika shida.
Kama binadamu, tunapaswa kushikamana: “Sisi sote ni kitu kimoja katika Bwana, matajiri na mafukara, watumwa na watu huru, wenye afya na wagonjwa pia; na mmoja ndiye kichwa kinachotegemewa na vyote: Yesu Kristo. Ni kama vile kwa viungo vya mwili mmoja, kila kimoja kinashughulikia kingine, na vyote kwa vyote. Huu ndio wokovu pekee kwa mwili wetu na roho yetu: kuwatendea kwa upendo… Ukiwa mzima na tajiri, punguza shida za yeyote aliye mgonjwa na fukara; kama hujaanguka, nenda kumsaidia yeyote ambaye ameanguka na anaishi kwa mateso; ukiwa na furaha, umfariji yeyote mwenye huzuni; ukiwa na hali njema, umsaidie yeyote aliyepigwa na mabaya. Umthibitishie Mungu shukrani yako kwa kuwa unaweza kusaidia, si mtu wa kuhitaji msaada… Uwe tajiri si kwa mali tu, bali pia kwa huruma; si kwa dhahabu tu bali pia kwa uadilifu, au afadhali kwa uadilifu tu. Zidi sifa ya jirani yako kwa kujionyesha mkarimu kuliko wote; ujifanye Mungu kwa wenye mashaka, ukiiga huruma ya Mungu”.

Sala yake

Ee Bwana, umpokee mikononi mwako kaka yangu aliyetuacha.
Kwa wakati wake utupokee sisi pia, kisha kutuongoza katika hija ya duniani hadi lengo ulilotupangia.
Utujalie tuje kwako tukiwa tayari na watulivu kweli, si tumevurugwa na hofu, si katika hali ya uadui nawe, walau siku ya mwisho, siku ya kufariki kwetu.
Utujalie tusijisikie tunaondolewa na kung’olewa kwa nguvu katika ulimwengu na maisha, wala kwa hiyo tusifunge safari shingo upande.
Bali utujalie tuje kwa utulivu na utayari mzuri, kama watu wanaoondoka kuendea uzima wa heri usio na mwisho, uzima ule ulioma katika Kristo Yesu, Bwana wetu, ambaye apate utukufu milele na milele. Amina.

Maandishi


Kaburi la Gregori katika Basilika la Mt. Petro huko Vatikano
  • Hotuba za kiliturujia.
  • Hotuba mbalimbali
  • Hotuba za kiteolojia
  • Barua 245
Vyanzo
Viungo vya nje
 
Yohane Krisostomo
 
 
 
 
Yohane Krisostomo, kwa Kigiriki χρυσόστομος, khrysóstomos, yaani «Mdomo wa dhahabu» alivyoitwa kutokana na ubora wa mahubiri yake, (Antiokia wa Siria, leo Antakya,nchini Uturuki, 347 hivi - Comana Pontica, Uturuki, 14 Septemba 407) alikuwa Patriarki wa Konstantinopoli.
Ari yake ilisababisha apendwe na vilevile achukiwe sana. Hatimaye alifukuzwa na Kaisari na kufa uhamishoni.
Tangu zamani anaheshimiwa kama mtakatifu na babu wa Kanisa.

Maisha

Asili na ujana

 

Yohane alizaliwa Antiokia wa Siria katika familia tajiri ya Kikristo mwaka 347 hivi. Wakati huo mji huo ulikuwa unamfuata Konstantinopoli na Aleksandria tu kwa umuhimu upande wa mashariki wa Dola la Roma.
Katika karne IV huko zilitokea vurugu nyingi kwa msingi wa dini. Mjini kulikuwa na maaskofu wawili walioshindana: Melesyo na Paulino. Yohane aliishi ujana wake katika mazingira hayo, akikosa utulivu, akipenda vyakula na maigizo.
Baba yake, Sekundo, aliyekuwa askari kiongozi, alifariki mapema na kumuacha mtoto mdogo pamoja na dada yake kwa mama yao, Anthusa, mwenye umri wa miaka 22 tu ambaye alimlea vizuri sana upande wa utu na wa imani vilevile.
Baada ya masomo yote, alifundishwa tena na Libanio, mhubiri maarufu kuliko wote wa wakati ule ingawa Mpagani, ambaye alisema juu yake, «Angekuwa kati ya wanafunzi wangu bora, kama Kanisa lisingeniibia». Kumbe Yohane akaja kumzidi, ila upande wa kuhubiri Neno la Mungu.
Alipofikia miaka 18 anni alikutana na askofu Melesyo akamuomba ubatizo (alioupata mwaka 368) akaanza kufuata kozi za Diodoro wa Tarso, maarufu kwa ufafanuzi wa maneno yenyewe ya Biblia usiofuata sana maana ya kiroho.

 

Kupewa daraja


Alipomaliza masomo hayo (367-372) na kupewa daraja ndogo akajifungia upwekeni miaka minne akasoma teolojia, hasa Injili na Nyaraka za Mtume Paulo. Katika pango alimoishi miaka miwili tena, afya yake ikawa mbovu ikamrudisha Antiokia kwenye wito wake halisi: uchungaji. Uzoefu wa kutafakari Neno la Mungu upwekeni ulikuwa umestawisha ndani yake msukumo mkubwa wa kushirikisha wengine kwa kuhubiri Injili.
Alitunga kitabu juu ya upadri kilichoathiriwa sana na Gregori wa Nazianzo. Humo alieleza kuwa umonaki si njia pekee ya kulenga ukamilifu; bali kutoa huduma za kipadri kwa faida ya waamini kati ya vishawishi vingi vya ulimwengu ndiyo njia bora ya kumtumikia Mungu. Aliandika kwamba angetakiwa kuchagua kati ya matatizo ya kuongoza Kanisa na utulivu wa maisha ya kimonaki angechagua mara elfu huduma ya kichungaji.
Miezi ya baridi kati ya miaka 380381 alipewa na Melesyo daraja ya ushemasi mwaka 386 na miaka michache baadaye akawa kasisi na msaidizi mkuu wa askofu Flaviano, akihubiri katika kanisa muhimu zaidi la Antiokia.
Wakati huo alisema, “Anatosha mtu mmoja mwenye ari kwa kubadilisha mwenendo wa umati”. Maneno hayo yakawa kaulimbiu yake kama mchungaji na kiongozi wa kiroho wa watu wake akiwatia moyo kufuata maadili.
Sifa yake kama mhubiri iliongezeka, hasa Antiokia ilipokabili ghadhabu ya Kaisari kwa uasi wa mwaka 387, hata wasikilizaji wakaanza kujiandikia kumbukumbu za maneno yake.
Pamoja na hayo mwenyewe aliendelea kutunga vitabu mbalimbali.
Mwaka 397 Patriarki Nektario alipofariki, kulikuwa na ushindani mkubwa kwa kushika nafasi yake, mpaka Kaisari Arcadio, kinyume cha matarajio ya wote, alipomchagua Yohane, ambaye hakuwa na hamu hiyo.
Alihamia huko kwa kutumiwa tu nguvu na udanganyifu, bila kujua namna ya kuhusiana na vigogo.

 

Askofu

 

Huko Konstantinopoli aliongoza Kanisa kwa bidii nyingi ili kulirekebisha, akishambulia ufisadi na anasa ya viongozi, akijipatia hivyo maadui wengi kwenye ikulu. Hivyo maisha yake hayakuwa na amani, tofauti na hamu ya moyo wake mpole.
Mwenyewe aliishi kwa usahili, unyenyekevu na uchangamfu kama kielelezo kwa wote, akitumikia watu na kutumia mali zake kwa ajili ya mafukara na wagonjwa.
Aliendelea kushika maisha magumu na kudai wasaidizi wake pia wafanye vilevile. Kwa usimamizi wake mzuri alianzisha na kuendesha miundo mbalimbali ya misaada, hata akaitwa “Mtoasadaka”.
Isitoshe, katika mahubiri yake alipendekeza Kanisa la Konstantinopoli lifuate kielelezo cha lile la kwanza la Yerusalemu na hivyo lichangie ujenzi wa jamii mpya ambapo wote waishi kama ndugu: hakuna wa kuachwa nyuma, kwa kuwa kila mmoja ni muhimu, si jamii tu. Hivyo alichangia sana mafundisho ya Kanisa kuhusu masuala ya jamii.
Kama mchungaji halisi, aliwatendea wote kwa wema, akiheshimu wanawake kwa namna ya pekee na kuwajibika kwa ustawi wa ndoa na familia.
Alihimiza waamini washiriki katika liturujia, aliyoipamba kwa ubunifu izidi kupendeza.
Alipambana kwa nguvu na uzushi na kuleta nidhamu katika majimbo yaliyo chini yake, akiwafukuza mapadri wengi wasiofaa, na hata askofu wa Efeso na wengine watano waliopata madaraka kwa dhambi ya usimoni. Kwa hilo alilaumiwa kuwa alitumia mamlaka nje ya mipaka yake.
Pia alilazimisha wamonaki wazururaji warudi katika monasteri zao, ila alipokea wengine kutoka Misri waliokuwa wametengwa na Kanisa kwa uamuzi wa Patriarki Teofilo wa Aleksandria, ambaye alichukia hilo pia.
Mwanzoni alitegemezwa na ikulu, lakini baada ya kumlaumu malkia Eudoksia kwa kujipatia mali ya mjane na kuishi kwa anasa, uhusiano uliharibika, akazidi kusingiziwa na kutukanwa.
Mwaka 402 maadui wake wengi, wakiwemo maaskofu, waliomba msaada wa patriarki Teofilo wa Aleksandria, ambaye Kanisa lake lilikuwa na ushindani na yale ya Konstantinopoli na Antiokia. Teofilo mwenyewe alikuwa amelazimika kujitetea katika sinodi iliyoongozwa na Yohane kuhusu mashtaka ya wamonaki dhidi yake.
Basi, mwaka 203 katika sinodi ya Mwaloni, karibu na Kalsedonia, Teofilo alifika pamoja na maaskofu saba wa Misri na wengine 29 waliokuwa wote upande wake, akamfanya Yohane afukuzwe na Kaisari, ila kesho yake malkia alimrudisha baada ya umati kudai hivyo kwa nguvu.
Miezi miwili baadaye uhusiano wa Yohane na Eudoksia ulichafuka tena, askofu alipolaumu ujenzi wa sanamu ya malkia karibu na kanisa, hata alisema maadhimisho kwa ajili yake yalikuwa ya kipagani akamfananisha na Herodia mwenye hamu na kichwa cha Yohane Mbatizaji.
Hivyo masingizio na njama viliendelea hata aliomba msaada wa Papa Inosenti I na maaskofu wengine muhimu wa magharibi, lakini huo haukuweza kuwahi: mtaguso, uliotakiwa na Kanisa la Roma ili kupatanisha pande mbili za Dola na makanisa yake yote, haukuweza kufanyika.

 

Uhamishoni

 

Basi, tarehe 9 Juni 404 Yohane alifukuzwa jimboni moja kwa moja. Kwa miaka mitatu aliishi Kukuso, kwenye milima ya Armenia, akitenda kazi kubwa hata kwa kuandika barua nyingi ili kuwatia moyo wafuasi wake waliodhulumiwa vilevile.
Halafu mwaka 407, kutokana na wingi wa watu waliomtembelea, alihamishwa tena aende mahali pagumu zaidi, huko Pitiunte, mashariki kabisa kwa Bahari Nyeusi, lakini tarehe 14 Septemba 407 alifariki huko Comana Pontica akiwa njiani.
Maneno yake ya mwisho yalikuwa: "Utukufu kwa Mungu kwa yote. (Doxa to Theo pantôn eneke)."
Mwaka 438 Kaisari mwingine, Theodosi II alirudisha masalia yake Konstantinopoli ambako yalipokewa na umati kwa shangwe.
Maandishi yake ni mengi sana, kuliko ya mababu wengine wote wa Kigiriki. Sehemu kubwa ni mahubiri (zaidi ya 700) aliyoyatoa kwa kawaida wakati wa liturujia, vitabu vya ufafanuzi wa Biblia, vya teoloja n.k. mbali ya barua 241 zilizotufikia.

 

Teolojia yake

 

Kama alivyopendekeza mwenyewe kwa waamini wake baada ya yeye kupelekwa uhamishoni, tunaweza kujilisha maandishi yake badala ya kumsikia akihubiri.
Kwa jumla hakuwa mwanateolojia mwenye mwelekeo wa nadharia, bali wa kichungaji, akilenga daima maisha yaendane na mawazo na maneno. Ndiyo mada kuu ya katekesi zake bora kwa waliojiandaa kubatizwa. Akikaribia kifo, aliandika kwamba thamani ya binadamu inategemea “ujuzi sahihi wa mafundisho ya kweli na unyofu wa maisha”: hayo mawili yanatakiwa kuendana.
Aliendeleza mapokeo ya Kanisa na kutoa mafundisho ya kuaminika wakati wa fujo kuhusu imani.
Alifundisha “kujua viumbe kuanzia Muumba”, ili viwe kama ngazi ya kumfikia. Zaidi ya hayo, kwa kuwa kwetu ni vigumu kufanya hivyo, Mungu mwenyewe alijishusha akatupa Maandiko matakatifu kama barua inayokamilisha ujuzi wetu juu yake. Isitoshe, alitwaa mwili akawa kweli “Mungu pamoja nasi”, ndugu yetu hata kifo chake msalabani. Hatimaye yeye anaingia maisha yetu kwa njia ya Roho Mtakatifu ili kutugeuza kwa ndani.
Kuhusu Kristo, Yohane alimkiri Mwana kuwa na hali moja na Baba. Pia kwamba alizaliwa na Maria, bikira kabla ya kujifungua, wakati wa kujifungua na baada ya kujifungua.
Anaitwa pia “Mwalimu wa Ekaristi” kutokana na upana na utajiri wa mafundisho yake kuhusu sakramenti ya Mwili na Damu ya Kristo.

Vyanzo 
Viungo vya nje 
Maandishi yake 
Vinginevyo

Kanisa la Orthodox na Kanisa Katoliki 
Umonaki katika Kanisa la Orthodox
Église orthodoxe Pères, la richesse et le capitalisme

Basili Mkuu na Yohane Krisostomo :

SS. Basile et Jean Chrysostome

Δεν υπάρχουν σχόλια:

Δημοσίευση σχολίου